• Thu. Apr 25th, 2024

Hamna la Kusherehekea Wakenya Walalamika Madaraka Dei

Jun 1, 2021
366 300

Huku Rais Kenyatta na Viongozi wa tabaka mbali mbali wakiongoza sherehe za madaraka katika Uga wa Jomo Kenyatta kaunti ya Kisumu, wakenya katika kaunti mbali mbali wanasema hawana chochote cha kusherehekea.

Wakizungumza katika mji wa Eldoret kaunti ya Uasin Gishu, wamesema kuwa kwa sasa hawana jambo la kufurahia ikizingatiwa kwamba uchumi umeharibika tokea mwaka jana baada ya janga la Korona kuingia nchini.

“Uchumi umezorota Sana. Tumeona bei ya Mafuta imepanda mara mbili sasa. Biashara ya matatu imekuwa mbaya Sana. Kuongezea tulikatazwa kubeba kama gari limejaa,” alisema dereva wa matatu.

“Mimi siwezi funga biashara yangu eti nasherehekea Madaraka. Nina familia inayonihitaji. Majukumu ni mengi tokea janga la Korona kuingia nchini,”mfanyibiashara mmoja alisema.

Hata hivyo wananchi hawa wameahidi kuendelea kuzingatia masharti yaliyowekwa na wizara ya afya katika kudhibiti kuenea kwa virusi vya Korona.

“Hali ni ngumu lakini tutazingatia masharti yaliyopo, ilikuhakikisha virusi hivi havisambai zaidi,” waliongeza.

Aidha, katika kaunti nyinginezo sherehe hazitaandaliwa kama ilivyo ada. Akizungumza na Taarifa News, kamshina wa Kaunti ya Samburu amewataka wananchi wa Kaunti hiyo kufuatilia sherehe zitakazokuwa zikiendelea katika kaunti ya Kisumu ambako Rais atahutubia taifa.

Na katika Kaunti ya Nyamira, wananchi wa huko wamesema kuwa hata kama sherehe zingeandaliwa katika kaunti yao, hawangehudhuria.

“Hata kama sherehe zingekuwa huku kwetu Mimi singehudhuria. Ningeendelea na biashara yangu tu. Siwezi enda kukaa huko na hakuna nitakacho pata au kupewa,”alisema Mkaazi wa Nyamira.

“Hata kukaa nyumbani na kufuatilia sherehe kwenye runinga ni bora ili kuzuia maambukizi ya virusi vya Korona,”aliongeza mwenzake.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *