Raila Odinga anatarajiwa kuzuru magharibi mwa Kenya kwa ziara ya kisiasa ya siku tano kama juhudi za kupigia debe azma yake ya kuwania kiti cha urais baadae mwaka huu. Ziara ya mgombea huyo wa urais kupitia tiketi ya Azimio La Umoja One Kenya itang’oa nanga kaunti ya Vihiga siku ya jumatano kabla ya kuelekea kaunti ya Transzoia siku ya alhamisi.
Odinga ambae hapo jana alitangaza vikosi 16 vitakavyo’ongoza kampeni za Azimio kutoka maeneo ya hapa nchini Kenya anatarajiwa kuandaa vikao na viongozi wa kisiasa kutoka magharibi mwa Kenya walio chini ya Azimio La Umoja One Kenya katika juhudi za kuimarisha mrengo huo.
Ziara ya kinara huyo wa chama cha ODM ni ya kwanza ukanda huo wa Mulembe Nation tangu kumteua Martha Karua kama mgombea mwenza na kumtangaza gavana wa Kakamega Wycliff Oparanya kama waziri wa fedha huku aliyekua mbunge wa Emukhaya Kenneth Marende akimtaja kama spika wa bunge la seniti iwapo Azimio itabuni serikali ijayo.
Kwa kile kinachoaminika kama kuendeleza umaarufu wake eneo hilo la magharibi mwa Kenya, Odinga anatarajiwa kuangazia maswala muhimu ikiwemo mpango wa Azimio La Umoja One Kenya kuboresha sekta za kilimo, afya, elimu na miundomsingi ikiwemo ujenzi wa mabarabara.
Swala kuu la kukabiliana na gharama ya juu bei ya mbolea na nafaka pia litaangaziwa sawia na mikakati ya Azimio kuhakikisha kila boma linapata maji baada ya uchaguzi wa Agosti 9.Vilevile kikosi cha Azimio kimeratibu kaunti za Busia na Bungoma kama baadhi ya maeneo watakazozuru hadi siku ya jumamosi wikendi hii.